ZDCEA NA DCEA ZAADHIMISHA SIKU YA KUPIGA VITA MATUMIZI NA BIASHARA HARAMU YA DAWA ZA KULEVYA DUNIANI.
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imekua ikichukua hatua mbalimbali katika kukabiliana na uhalifu wa dawa za kulevya sambamba na kuanzisha Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na dawa hizo nchini.
Hayo yamesemwa na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe. Hemed Suleiman Abdulla kwa niaba ya Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dkt Hussein Ali Mwinyi katika maadhimisho ya kilele cha siku ya kupiga vita matumizi na biashara haramu ya dawa za kulevya duniani hafla iliyofanyika katika ukumbi wa ofisi ya tume ya uchaguzi Maisara wilaya ya mjini unguja.
Amesema kuwa Zanzibar ikiwa nisehemu ya Dunia inaungana na Mataifa mengine katika kuadhimisha siku hii hivyo ni wajibu wa kila mmoja wetu kutambua kuwa matumizi ya dawa za kulevya ni tatizo linaloendelea kuyasumbua Mataifa yote duniani hususan vijana katika kila pembe ya dunia wanaendelea kujiingiza katika janga hili baya siku hadi siku.
Makamu wa pili wa rais wa Zanzibar amesema serikali imejipanga Kusambaratisha mitandao ya wahalifu wakubwa wa dawa za kulevya pamoja kutaifisha mali mbali mbali za wahusika wa dawa hizo wa ndani na nje ya nchi.
Mhe. Hemed amesema Serikali imeimarisha huduma za tiba na marekebisho ya tabia kwa kujenga vituo vya kutoa huduma kwa waathirika lakini bado inakabiliwa na changamoto mbalimbali ikiwemo, Mabadiliko ya mara kwa mara ya mbinu zinazotumiwa na wahalifu ikiwemo utengenezaji wa dawa mpya za kulevya zenye muundo tofauti na dawa za asili kama vile bangi, cocaine na heroine na zenye athari zaidi ya dawa za kulevya katika pipi, chocolate, biskuti na sigara za kiektroniki pamoja na Matumizi ya teknolojia katika biashara hiyo haramu pamoja na kuongezeka ushawishi kwa vijana kupitia mitandao ya kijamii.
Sambamba na hayo mhe hemed ametoa wito kwa wazazi, walezi, viongozi wa dini, walimu na jamii kwa ujumla kuendelea kusimamia malezi bora ya vijana pamoja na kuzikumbusha familia ambazo ndio msingi wa kwanza wa wa kinga dhidi ya dawa za kulevya, kuongeza juhudi za kuwekeza kwenye maadili, elimu na mawasiliano mazuri ndani ya familia kwani bila ya kufanya hivyo taifa litakosa nguvu kazi ya baadae.
Aidha, ameviagiza vyombo vinavyohusika na mapambano dhidi ya dawa ya kulevya kushirikiana na Mamlaka husika katika kuwafichua wahalifu wa dawa za kulevya na kuacha muhali.Â

